Kidugala, Njombe – tarehe 21 Novemba 2025
Katika ibada maalum iliyofanyika katika Usharika wa Kidugala, Jimbo la Kusini la KKKT limemsimika rasmi Mchungaji Amani Kabelege kuwa Mkuu wa Jimbo la Kidugala. Tukio hili la kihistoria lilihudhuriwa na viongozi wakuu wa kanisa, wachungaji wa sharika mbalimbali, pamoja na waumini kutoka sehemu mbalimbali za jimbo.
Ibada hiyo iliongozwa na Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kusini Mhashamu Dk George Mark Fihavango akisaidiana na Msaidizi wa Askofu Mhashamu Dk Johnson Lunanilo Gudaga. Viongozi wengine waliojiunga na ibada hiyo ni Mkuu wa Seminari ya Kilutheri ya Kidugala, Mchungaji Wallace Lupenza pamoja na wachungaji wa sharika za jimbo la Kidugala.

